TANZANIA NA RWANDA ZAPIGA HATUA NYINGINE UJENZI WA SGR ISAKA-KIGALI - TRC Blog

Home Top Ad

"TOGETHER WE MOVE"

Friday, January 26, 2018

TANZANIA NA RWANDA ZAPIGA HATUA NYINGINE UJENZI WA SGR ISAKA-KIGALI

Tanzania na Rwanda zapiga hatua nyingine katika ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) yenye urefu wa km521 kutoka Isaka hadi Kigali baada ya mawaziri wa uchukuzi wa chi hizo mbili kukutana siku ya tarehe 20 January 2018 jijini Dar es Salaam kujadili namna ya kutekeleza mradi huo kufuatia agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli la kukutana kwa mawaziri hao wawili mapema.
Katika mkutano huo waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Prof. Makame Mbarawa na waziri wa Miundombinu wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. James Musoni walijadili na kutoa mapendekezo ya namna ya utekelezaji wa mradi huo.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Prof. Makame Mbarawa na Waziri wa Miundombinu wa Rwanda Mhe. James Musoni baada ya kusaini makubaliano ya ushirikiano wa pamoja.
Mkutano huo uliofanyika jijini Dar es Salaam kwenye ofisi za Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ulihudhuriwa pia na mawaziri kutoka Tanzania akiwemo Waziri ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Africa Mashariki Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mipango na Fedha, Dkt. Philip Mpango, Balozi wa Jamhuri ya Rwanda nchini Tanzania Mhe. Eugene Kayihura, makatibu wakuu wa Wizara za uchukuzi wa nchi za Rwanda na Tanzania pamoja na maafisa waandamizi wengine kutoka nchi hizo mbili.
Mawaziri wa nchi hizo mbili wameeleza kuwa wamejitoa kuhakikisha ushirikiano na mahusiano ya kibiashara katika nchi hizo mbili unakua, lengo likiwa ni kukuza uchumi na kuziletea maendeleo nchi hizo mbili, kwakuwa kukamilika kwa ujenzi wa reli hiyo ya Isaka-Kigali kunatarajiwa kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo na kuongeza kiasi cha mizigo inayosafirishwa kwenda nchini Rwanda kupitia Bandari ya Dar es Salaa.
Mawaziri hao wawili wamekubaliana kutumia upembuzi uliofanywa katika nchi hizo mbili katika kipindi kilichopita kujenga reli inayofanana na inayojengwa kutoka Dar-Morogoro hadi Makutupora kwa lengo la kuwa na viwango stahiki vinavyofanana.
Makubaliano ya ushirikiano wa pamoja yalisainiwa na Waziri wa Miundombinu wa Rwanda Mhe. James Musoni na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wa Tanzania Prof. Makame Mbarawa, makubaliano yaliyolenga kuunganisha nguvu katika ujenzi wa reli hiyo ambapo kila nchi itagharamia ujenzi wa reli hiyo ya kisasa katika eneo lake.  



No comments:

Post a Comment