TRC YASAINI RASMI MKATABA WA UNUNUZI WA VICHWA 11 VYA TRENI VILIVYOKO BANDARINI - TRC Blog

Home Top Ad

"TOGETHER WE MOVE"

Friday, March 16, 2018

TRC YASAINI RASMI MKATABA WA UNUNUZI WA VICHWA 11 VYA TRENI VILIVYOKO BANDARINI

Mkurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania Ndg. Masanja Kungu Kadogosa leo tarehe 16 Machi 2018 amesaini mkataba na Kampuni ya Progress Rail Locomotives (PRL) ya Marekani inayomiliki vichwa vya treni 11 vilivyoletwa katika Bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya kuvinunua vichwa vyenye namba 9014, 9015, 9016, 9017, 9018, 9019, 9020, 9021, 9022, 9023 na 9024.           

Mnamo mwezi Julai 2017, Kampuni ya Progress rail Locomotives (PRL) ya Marekani ilileta vichwa vya treni 11 katika Bandari ya Dar  es salaam kwa ajili ya kuviuza vyenye namba  9014, 9015, 9016, 9017, 9018, 9019, 9020, 9021, 9022, 9023 na 9024.           
Tarehe 27 Septemba, 2017 Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa aliteua kamati ya wataalamu kwa ajili kubaini kama vichwa hivyo ni vipya au la. Wajumbe wa kamati hiyo walitoka chuo kikuu cha Dar es salaam, TEMESA na Shirika la Reli  Tanzania(TRC). Kamati hiyo ilifanya kazi hadi 15 oktoba,2017 na kukabidhi ripoti kwa Mheshimiwa Waziri. Kamati ilibaini kuwa vichwa hivyo vya treni ni vipya.
Mkurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania Ndg. Masanja Kadogosa akibadilishana makabrasha na mwakilishi wa Kampuni ya Progess Rail Locomotive mara baada ya kusaini mkataba wa ununuzi wa vichwa 11 vya treni.
Aidha tarehe 16 Oktoba, 2017 Mheshimiwa Waziri kwa mara nyingine aliteu akamati ya wataalamu wenye taaluma mbalimbali wakiwemo wanasheria wahandisi na wachumi kwa ajili ya kujadiliana bei ya kuvinunua vichwa hivyo. 
Awali mwaka 2015, Serikali ilinunua vichwa kama hivyo 13 vyenye namba  9001, 9002, 9003, 9004, 9005, 9006, 9007, 9008, 9009, 9010, 9011, 9012 na 9013 kwa bei ya dola za kimarekani Milioni 3,200,000 kwa kichwa kimoja. Kamati hivyo ilifanya majadiliano ya bei na kufikia muafaka wa kununua kwa dola za kimarekani milioni 2,400,000 kwa kichwa kimoja ambavyo ni pungufu ya dola 800,000 kwa kila kichwa cha treni kulinganisha na bei ya vichwa tulivyonunua awali, kwa maana hiyo kwa vichwa 11 serikali imeokoa dola  8,800,000.
Majaribio yatakuwa katika awamu tatu. Kwanza ni ukaguzi kwa kuvitizama(visual inspection), pili ni kuviwasha na kuvipa mizigo vikiwa havitembei(load box) na tatu ni kufunga na kuvuta mzigo wa tani 700 toka Dar es salaam hadi Morogoro na tani 1200 toka Morogoro hadi Kigoma na Mwanza. 
Ununuzi wa vichwa hivi 11 utaongeza ufanisi wa shirika kwani kwa sasa hivi tunavyo vichwa 29 madhubuti kati ya vichwa 47 tunavyovihitaji ilikutoa huduma nzuri kwa wateja wetu.


Mkurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania Ndg. Masanja Kadogosa  akizungumza na waandishi wa habari kabla ya kusaini mkataba wa ununuzi wa vichwa 11 vya treni na kampuni ya Progress Rail Locomotives ya Marekani
Mkurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania Ndg. Masanja Kadogosa  na mwakilishi wa Kampuni ya Progess Rail Locomotive wakisaini mkataba wa ununuzi wa vichwa 11 vya treni.
Mwanasheria wa Shirika la Reli Tanzania  na mwakilishi wa Kampuni ya Progess Rail Locomotive wakisaini mkataba wa ununuzi wa vichwa 11 vya treni.



No comments:

Post a Comment